Polisi kaunti ya Kisii wanamzuilia mwanamke mmoja kwa tuhuma za mauaji ya mfanyakazi wa duka moja mjini humo jioni ya jana.
James Kuria mwenye umri wa miaka 36, mhasibu katika duka la jumla la Shivling, alipigwa visu na kuuawa na Hellen Atieno ,30, saa kumi na moja jioni ya jana.
Kuria alitangazwa kufariki alipofikishwa katika Hospitali ya Mafunzo na Rufaa ya Kisii.
Mshukiwa pia ni mfanyakazi katika duka hilo na alifanya kazi kama msaidizi wake katika idara ya fedha.
Ripoti ya polisi ilisema kuwa wawili hao walikuwa na ugomvi kabla ya marehemu kumpiga kofi dada huyo, ambaye naye alichukua kisu na kumdunga mara kadhaa.
Haijulikani ikiwa kisu cha mauaji kilichokotwa kwenye rafu au alikuwa nacho kwenye mkoba wake.
Mmiliki wa duka kuu la Shivling Rajesh Patel, alisema kuwa tayari wametuma taarifa zote zinazohitajika kwa polisi kwa uchunguzi.
Kisu cha mauaji kilipatikana katika eneo la tukio na maafisa wa upelelezi kutoka kituo cha Polisi cha Kisii Central.
Leave a Comment