HARRY Kane alifunga bao lake la 250 ndani ya jezi za Tottenham Hotspur mnamo Jumamosi na kusaidia kikosi hicho kukomoa Wolves 1-0 katika Ligi Kuu ya Uingereza (EPL).
Kane alicheka na nyavu za wageni wao katika dakika ya 64 baada ya kushirikiana vilivyo na sajili mpya wa Spurs, Ivan Perisic.
Bao hilo la Kane lilifanya Spurs kuwa kikosi cha tano kuwahi kufunga mabao 1,000 mbele ya mashabiki wao wa nyumbani tangu kipute cha EPL kianzishwe mnamo 1992.
Mbali na Kane, 29, mchezaji mwingine aliyeridhisha zaidi kambini mwa Spurs ni mshambuliaji Son Heung-min aliyeshuhudia makombora yake mawili katika kipindi cha kwanza yakigonga mwamba wa lango la Wolves.
Chini ya kocha Bruno Lage, Wolves walianza pambano hilo kwa matao ya juu huku wakilinda vilivyo ngome yao na kushambulia Spurs kupitia kwa Matheus Nunes na Ruben Neves. Hata hivyo, walipoteza nafasi nyingi za wazi huku wakiendeleza rekodi ya kutoshinda mechi kati ya 10 zilizopita.
Licha ya kulazimika kusubiri hadi katikati ya Oktoba kabla ya kufunga bao lake la kwanza katika EPL mnamo 2021-22, Kane kwa sasa amepachika wavuni mabao mawili muhimu katika mechi tatu ambazo zimetandazwa na Spurs chini ya kipindi cha mwezi mmoja.
Bao la sekunde za mwisho alilofunga dhidi ya Chelsea ugani Stamford Bridge wiki moja iliyopita liliwezesha Spurs ya kocha Antonio Conte kuendeleza rekodi ya kutoshindwa katika EPL msimu huu.
Leave a Comment