Mshambuliaji matata Robert Lewandowski alifungia daftari lake la Barcelona kwa kufunga mabao mawili katika ushindi wao wa 4-1 dhidi ya Real Sociedad katika Ligi Kuu ya Uhispania mnamo Jumapili, Agosti 21.
Lewandowski ambaye alikuwa anaadhimisha miaka 34 tangu kuzaliwa, aliipa Barcelona uongozi baada tu ya sekunde 50 kabla ya Alexander Isak kuwasawazishia wenyeji Real Sociedad.
Kocha wa Barcelona Xavi alimwingiza mshambuliaji Ansu Fati ambaye aliwaandalia Ousmane Dembele na Lewandowski bao moja kila mmoja kabla ya kutikisa wavu mwenyewe.
Ushindi wa kwanza wa Barcelona wa msimu unajiri baada ya kufungua msimu kwa sare ya 0-0 dhidi ya Rayo Vallecano wikendi iliyopita ugani Camp Nou.
Alejandro Balde mwenye umri wa miaka 18 alimpa krosi ya sakafuni Lewandowski ambaye aliupachika wavuni mpira huo hata kabla watu hawajatulia uwananj lakini Sociedad wakasawazisha katika dakika ya sita baada ya Frenkie de Jong kupoteza mpira katikati mwa uwanja. Sociedad walikuwa wamebaba hadi Fati alipoingizwa na Xavi katika dakika ya 64 na mchezo huo kubadilika.
Fati mwenye umri wa miaka 19 alishirikiana vizuri na Dembele na kuleta bao baada tu ya dakika mbili kabla tena ya kumpakulia Lewandowski. Fati ambaye ameandamwa na majeraha katika misumu miwili iliyopita baada ya kuingia katika kikosi cha kwanza, alitikisa wavu naye pia baadaye baada ya kuupokea mpira kutoka kwa Lewandowski
Leave a Comment